Serikali kupitia Wizara ya Afya,Maendeleo ya Jamii,Jinsia, Wazee na watoto imewataka watoa huduma za afya nchini kutokuwasahau watoto na vijana katika kuwakinga na maambukizi ya Virusi Vya Ukimwi (VVU).
Hayo yamesemwa na Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt. Faustine Ndugulile wakati wa uzinduzi wa Mkakati wa wauguzi na wakunga kusogeza huduma za VVU na UKIMWI karibu na jamii ikiwemo ushauri nasaha, kupima VVU na kufuatilia maendeleo ya afya za walengwa uliofanyika mapema leo mkoani Njombe.
“Bado tuna changamoto kwa watoa huduma wetu wa afya kwa baadhi ya maeneo ikiwemo kutokuwapima watoto hali ya maambukizi, kutoa dawa kwa watoto na kuwapa elimu vijana hivyo natoa rai kwa wahudumu wa afya tuweze kuweka mkakati wa kufikia makundi hayo” alisema Dkt. Ndugulile.
Aidha Dkt. Ndugulile amewasisitiza Wauguzi na Wakunga kutoa huduma kwa kuzingatia miiko na maadili hususan katika kutoa huduma za VVU kwa jamii inayowazunguka ikiwemo kutumia lugha nzuri na kuwa wanyenyekevu kwa wananchi.
Sambamba na hilo Dkt. Ndugulile amewaasa wanaume nchini kuacha uoga na kujitokeza kupima VVU ili kutambua afya zao na kuanza matibabu mara moja iwapo watakutwa na maambukizi.
“Tutawafuata wanaume popote walipo hususan waliopo kwenye mikusanyiko yao ikiwemo kwenye sehemu za starehe, viwanja vya mipira , Migodini na sehemu za uvuvi ili kutoa elimu na kuwashauri wapime ili kujua afya zao” alisema Dkt. Ndugulile.
Aidha Dkt. Ndugulile amesema kusudio la kufanya hivyo ni kuhakikisha kufikia malengo ya 90 90 90 ya kutokuwa na maambukizi mapya ifikapo mwaka 2030. Ambapo asilimia 90 ya watu wanaoishi na virusi vya Ukimwi wawe wanajua hali zao za maambukizi.
Ili kutimiza malengo ya serikali katika kupambana na maambukizi, Dkt Ndugulile amesema Serikali imekuja na utaratibu wa dawa kinga ambapo dawa hizo zitatumika kwa makundi maalumu ambayo yako hatarini kupata maambukizi.
“Lakini vile vile tumekuja na utaratibu unaoitwa dawa-kinga ambazo kuna makundi ambayo tumebaini, ambayo yako kwenye hatari kubwa ya kupata maambukizi ya UKIMWI. Makundi haya kuna dawa ambayo tunataka tuwape zisaidiane na kinga nyingine ili kusaidia watu wasipate maambukizi ya virusi vya UKIMWI lakini hatusemi kwamba tumeshapata kinga”. Dkt Ndugulile.
Sambamba na hayo Dkt. Ndugulile amewataka watoa huduma waende wakatoe msisitizo na kuelimisha jamii katika maeneo ambayo dawa-kinga zimeanza kufanyiwa majaribio ili kuleta matokeo chanya.
Kwa upande wake Mkuu wa Mkoa wa Njombe Christopher Ole Sendeka amesema ukanda wa nyanda za juu kusini ni ukanda ambao una maambukizi makubwa ya VVU na serikali ya mkoa ilianza kampeni ya tohara kwa wanaume, na sasa inaelekea kwa watoto wa sekondari na shule ya msingi ikiwa ni njia mojawapo ya kupambana na maambukizi mapya.
“Takwimu zinaonesha sisi tuna kiwango kikubwa cha maambukizi kuliko katika ukanda ule ambao tohara kwa wanaume inaanzia katika umri mdogo kiwango cha maambukizi kiko chini lakini pia kuna mahusiano kati aya tohara ya wanaume na maambukizi ya VVU kwahiyo kama mkoa kampeni hii tumeivalia njuga chini ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto na TAMISEMI”. Alisema Ole Sendeka.
Uzinduzi huo ulihudhuriwa na Waganga Wakuu wa mikoa na Wafawidhi wa mikoa mbalimbali pamoja na wauguzi na wakunga waliopata muongozo wa kusogeza huduma za VVU na UKIMWI karibu na jamii ikiwemo ushauri nasaha, kupima VVU na kufuatilia maendeleo ya afya za walengwa.
Christopher philemon
Afisa habari Mkoa wa Njombe
Mtaa wa Lunyanywi
Postal Address: P.O.Box 668-Njombe
Telephone: 026 278 291 213
Mobile:
Email: ras@njombe.go.tz
Copyright ©2019 GWF . All rights reserved.